Sunday, February 24, 2013

HISTORIA YA MTWARA


Na Cosmas J. Pahalah

Mkoa wa Mtwara ni wapili kwa udogo baada ya Mkoa wa Kilimanjaro.Jina la Mtwara limetokana na neno la lugha ya kimakonde “kutwala” ikiwa na maana ya kuchukua(kunyakua) kitu chochote na linatumika kwa maeneo matatu tofauti ambayo ni:
Mtwara Jina la Mkoa, Mtwara-Jina la mji mkuu na makao makuu ya Mkoa, Mtwara-Wilaya na makao makuu ya Wilaya ambayo kiutawala kuna Mtwara vijijini na Mtwara Mikindani
Wakati wa utawala wa Waingereza Tanganyika ilikuwa na majimbo 8. Mkoa wa Mtwara umechotwa kutoka eneo kubwa la Tanzania ambalo wakati wa utawala wa Waingereza liliitwa jimbo la kusini. Jimbo la kusini lilijumuisha Mikoa mitatu ya sasa Lindi,Ruvuma na Mtwara.
Jimbo la Kusini lilijumuisha Wilaya 8 ambazo ni Mtwara, Newala, Masasi, Lindi, Kilwa, Nachingwea, Tunduru na Songea.
 Mkoa wa Ruvuma ndio ulikuwa wa kwanza kugawanywa toka Jimbo la Kusini mnamo miaka ya 1960. Mwaka 1971 Jimbo la Kusini liligawanywa tena na kuundwa rasmi kwa Mikoa ya Mtwara na Lindi.
Mtwara ikiwa na Wilaya 3 kwa wakati huo ambazo ni Mtwara, Newala na Masasi. Kwa sasa Mtwara inaundwa na Wiliya 5 ambazo ni Mtwara, Newala, Masasi, Tandahimba na Nanyumbu. Makabila yaliyokuwemo katika jimbo hilo ni wangoni ,wamatengo, wandendeule ,wamatumbwi, wamwera,wamagingo,wamakonde,wayao na wamakua ambayo yamekuwa na uhusiano mrefu wa jadi na nyingi za mila na desturi zao kwa ujumla zinalingana mno.
Baada ya kuundwa kwa Mkoa wa Mtwara makabila makubwa matatu yanayopatikana ni Wamakonde, Wamakua na Wayao wanaopatikana katika Wilaya tofauti za Mkoa huu. Hata hivyo Wamakonde wanapatikana zaidi katika Wilaya za Newala na Mtwara, Wamakua na Wayao wanapatikana zaidi Wilaya ya Masasi.
 


Kusini chini ya Waingereza
Baada ya Wajerumani kuangushwa duniani pote katika Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia (1914 – 1918), Tanganyika, iliyokuwa sehemu ya Dutch East Africa (nchi nyingine katika eneo hili zikiwa Rwanda na Burundi) iliwekwa chini ya utawala wa Waingereza kama wadhamini.

Nchi haikuwa koloni kama ilivyokuwa Kenya, Nyasaland( Malawi) na Northern Rhodesia (Zambia). Kwa maeneo ya kusini hali ilikuwa kama Wadachi waliwaambia cha kuwafanyia wenyeji wa kusini.
 Hakuna kumbukumbu zinazoonyesha kwamba watawala wapya walikuwa na mipango au azma ya kuendeleza eneo hilo katika fani mbali mbali. Yaliyotokea yalilenga kunufaisha watawala.
Baada ya vita Waingereza walikuwa wachovu kiuchumi hali ya huduma za kijamii ziliathirika na vita. Kampuni iliyoitwa Overseas Food Corporation ilianzisha mradi mkubwa wa kulima karanga Urambo (Tabora) Kongwa (Dodoma) na Nachingwea (Lindi).
 Ili kuhudumia mashamba kwa ufanisi bandari ya Mtwara iliboreshwa. Wakati huo huo wakajenga reli na bomba la mafuta toka bandarini Mtwara hadi Nachingwea. Reli ilikuwa ienddelee hadi Mbamba bay pwani ya ziwa Nyasa.
Mnamo mwezi Oktoba 1961 lilifunguliwa tawi la reli la kilomita takribani 40, toka Chilungula hadi Masasi.
 Miundombinu na shughuli za kilimo zilitoa ajira na maeneo yaliyopitiwa na miundo msingi hiyo yalifunguka kwa maendeleo

Kwa sababu mbali mbali mradi wa karanga Nachingwea ulifungwa. Mwaka mmoja baada ya Tanganyika kupata Uhuru, sarikali ya Tanganyika huru ikaamini kuwa reli na bomba la mafuta vilikuwa ni miradi isiyo na tija. (white elephant).

 Reli na bomba vikang’olewa. Athari za hatua hiyo ni bayana .Kusini kulizidi kuzama kimaendeleo, taswira iliyodumu kwa kipindi kirefu. Lakini kwa muda mfupi watawala (Waingereza) walimaizi kwamba eneo la kusini lilikuwa na utajiri mwingi hivyo wakaita “Cinderella Province” Cinderella ikiwa na maana ya ‘mtu au kitu ambacho uzuri au uwezo wake haujatambulikana”.
Jingine walilolifanya Waingereza ni kuangusha magogo na kupasua mbao huko Rondo Mnara (Lindi vijijini). Kampuni iliyoitwa Steel Brothers ilifanya kazi hiyo miaka ya 1950. Wakavuna , wakachuma na kuondoka . Wananchi wakaachiwa visiki vya mipingo , mbambakofi,mivule nk. wakati huo huo walikumbatia umasikini.

Kusini baada ya uhuru.

Miaka michache ya kuelekea uhuru kulianzishwa mradi mkubwa wa maji toka mto Ruvuma ,uliendeshwa na kampuni ya Makonde Water Corporation. Ilipangwa maji yaenezwe sehemu mbalimbali huko kusini. Miaka michache baada ya kuasisiwa kwa vishindo mradi ulikufa. Wananchi hawakuelezwa sababu za mabadiliko hayo.

Madhila,taabu na kero za kukosa maji hazikumilithika .
Katikati ya miaka 1960 kulizuka mgogoro wa kiwanja katika mji mdogo wa Mahuta (wakati huo Newala , sasa uko katika wilaya ya Tandahimba ).
Mfanyabiashara wa Kiasia alipora eneo hilo ili ajenge kituo cha mafuta ya nishati. Wananchi wakachachamaa. Uongozi wa mkoa na wilaya ukaingilia kati. Kwenye mkutano wa hadhara hapo Mahuta , kiongozi wa wananchi alipigwa viboko kwa sababu za “kupinga hatua za maendeleo “ kama walivyoita watawala.
Kupinga uonevu kunyanyaswa na kudharauliwa, wananchi waliandika barua ngazi za juu za taifa na kudai , moja , mkuu wa mkoa na yule wa wilaya wahamishwe ,mbili, wapendekeze majina ambayo yatatoa mkuu wa mkoa na yule wa wilaya ; na tatu kama maombi hayo hayatakubalika watajitenga na kujiunga na Msumbiji ili wawe pamoja na FRELIMO kutafuta ukombozi. Yaliyofuata ni historia.
Miaka mitatu baada ya uhuru wa Tanganyika , wana Msumbiji kupitia FRELIMO walianzisha vita vya ukombozi. Kutokana na mazingira ya kijiografia ( kati ya nchi mbili ) eneo lote la kusini likawa “no go area” – hapakuwa na shughuli zozote za maana za kimaendeleo zilizokuwa zikifanyika .
 FRELIMO wakafanikiwa kukunja jamvi ukoloni mwaka 1975. Ni dhahiri kwa miaka kumi wengine walikuwa wamesonga mbele hapa nchini . Mategemeo na matumaini ya wengi huko kusini ni kuwa serikali ingekuwa na programu maalum “kufidia muda uliopotea”. Wakati wa Vita kuu ya Pili vya dunia Yugoslavia ilipambana na majeshi ya Adolf Hitler .
Marshal Josef Tito akawaambia wapiganaji wale “ The wounded should not be left behind “ ( majeruhi wasiachwe nyuma). Kimaendeleo kusini ilijeruhiwa na kuachwa nyuma.
Barabara ya Dar es salaam – Lindi ni “mkunga” wa matatizo ya kusini.
Ahadi za serikali kuijenga zimechukua kipindi kirefu kutekelezwa. Miaka ya 1970 – 80 kampuni moja ya Kitanzania na taasisi moja ya serikali waliteuliwa kujenga barabara hiyo.
 Wakajenga makambi Nangurukuru (Kilwa).Hakuna ushahidi wa kazi iliyofanywa – tatizo la barabara likawa “ kichwa cha mwenda wazimu”. Mwaka 1977 wananchi wa kusini, wakiungwa mkono na wa maeneo mengine, waliasisi mchango maalum kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo. Mwitikio wa wito huo ulikuwa chanya.
Ofisini ya Waziri Mkuu ikasitisha zoezi hilo kwa ahadi kuwa serikali igejenga mradi huo. Imechukua miongo kadhaa kukamilika kazi hiyo.
Miaka ya 1960 – 70 wananchi wa kusini walihamasishwa kulima korosho kwa ajili ya biashara. Matokeo yalikuwa ya kutia moyo. Mapori yalipisha mashamba ya mikorosho. Zao likachangia umasikini. – Pembejeo bei juu na soko likawa halina uhakika .
Kuna viwanda vya kubangua korosho Masasi , Newala Lindi na Mtwara lakini hakuna msimamo maalum wa Bodi ya Korosho na wanasiasa wa kuuza nje zao lililoongezewa thamani. Bado wanakumbatia fikra hafidhina zilizopitwa na wakati wa kuuza nje ya nchi korosho ambazo hazijabanguliwa.

MAGONJWA HAYA CHANZO CHA MIKOROSHO KUDUMAA

KOROSHO ni zao muhimu la biashara katika nchi yetu kwani linampatia mkulima kipato na kuliingiza taifa fedha za kigeni zinazotokana na mauzo ya zao hilo ndani na nje ya nchi. Kwa kawaida miti ya mikorosho inastawi vizuri katika ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi. Zao hilo hapa Tanzania linalimwa na wakulima wadogo ambao wana miti mikorosho kati ya 60 mpaka 80.
Mikoa inayolima korosho ni Mtwara, Lindi, Pwani, Tanga na Ruvuma katika wilaya ya Tunduru. Mikoa mingine ambayo imeanza kulima korosho kwa kiwango kidogo katika maeneo yenye hali ya hewa inayofaa kwa kilimo cha zao hilo ni mkoa wa Mbeya, Njombe, Iringa, Morogoro, Dodoma, na Singida.
Uzalishaji wa juu wa korosho katika msimu wa mavuno wa mwaka 1973/74 ulifikia tani 145,000 za korosho ambazo kwa sehemu kubwa zilisafirishwa kwenda India.
Magonjwa ni kikwazo
Mbali na hayo zipo changamoto mbalimbali ambazo zinasababisha baadhi ya wakulima kukata tamaa kwa mfano kuwapo kwa ugonjwa unaoshambulia zao hilo.Mkoani Mtwara, kuna kituo cha utafiti wa magonjwa yanayoshambulia zao hilo cha Naliendele ambacho kinafanya utafiti ili kubaini magonjwa na wadudu waharibifu, na kutafuta ufumbuzi.
Dk Louis Kasuga ni mtafiti wa kituo hicho anasema ugonjwa wa Ubwiri, ulionekana ni tatizo kubwa katika kilimo cha korosho. Katika Miaka ya karibuni pia ugonjwa wa blaiti nao umeonekana kushambulia zaidi zao hilo na kwamba hivi sasa magonjwa hayo yamepatiwa dawa za kudhibiti magonjwa hayo.
Dk Kasuga anasema tatizo lingine ni gugu tegemezi (dodder) ambalo limekuwa likiota kwenye maeneo ya Mtwara, Lindi, Kilwa, Rufiji, Mkuranga, Bagamoyo, Pangani, Tanga na Mkinga. Gugu hilo ni chanzo chake ni mbegu iliyoota na kutegemea mmea mwingine kama miti ya mikorosho kustawi.
Utafiti uliofanywa na Kituo cha Naliendele kwa kikishirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam umethibitisha kuwa gugu hilo linastawi vizuri katika ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi. Dk Kasuga anasema mbali ya gugu hilo kushambulia mikorosho pia linashambulia mazao mengine kama michungwa, miti ya membe, mimea mingine.
Wakulima wanatambua kuwapo kwa tatizo hilo, lakini uelewa kuhusu chanzo cha tatizo hilo numekuwa ni utata na namna ya kudhibiti bado limekuwa ni kitendawili.
“Gugu hilo halina majani hivyo halina uwezo wa kujitengenezea chakula chake chenyewe, kwa msingi huo huishi kwa kutegemea mimea mingine ili liweze kupata chakula ikiwa ni pamoja na miti ya mikorosho,” anasema mtaalamu huyo.


Gugu lapunguza uzalishaji
Anasema gugu hilo linadumaza na kunyonya chakula cha mimea mingine na kwamba gugu hilo linaweza kusababisha mmea kufa au kukauka. Dk Kasuga anasema gugu hilo linasambaa kwa urahisi zaidi kwa njia ya upepo, maji, ndege, na wanyama. 
Anasema gugu hilo linapunguza uzalishaji wa korosho kwa asilimia 100 kwa sababu linategemea miti ya mikorosho kupata chakula. 
“Hii ni kwa sababu ya ushindani wa chakula, maji na jua naa gugu hilo linakuwa na lina nguvu kubwa ya kunyonya maji na chakula kutoka katika mti wa mkorosho, hali hiyo inapunguza kipato cha mkulima kutokana na kushuka kwa mavuno ya korosho,” anasema. Anasema gugu hilo linasababisha umaskini wa kipato na chakula katika kaya na kupunguza kipato cha fedha za kigeni kwa taifa. 
Anabainisha kwamba mbegu za gugu tegemezi zinauwezo wa kukaa chini ya ardhi kwa miaka kumi bila kupoteza uwezo wa kuota na hivyo linaonekana kuwa sugu. Kwa mujibu wa tovuti mbali mbali, mbegu za gugu tegemezi ni ngumu kufa kwani hata wanyama wakila na kutoa kinyesi zinauwezo wa kuota.

Dk Kasuga anasema njia za kudhibni gugu hilo ni kutoa kambakamba zake kwa kuzivuta, ingawa gugu hilo limekuwa likirejea kwenye mti uliopo karibu na gugu. Ofisa Kilimo wa Mkoa wa Pwani, Robinso Wanjara anasema uongozi wa Mkoa wa Pwani kwa kushirikiana na kituo cha utafiti cha magonjwa ya korosho kimewapa maelekezo maofisa kilimo ngazi za kata ili wakachungeze ukubwa tatizo hilo.
“Tunaamini kuwa wataalamu wetu tuliowatuma kwenda kwa wakulima watatuletea takwimu sahihi na kuzipeleka kwenye kituo cha Naliendele kwa ajili ya utafiti zaidi,” anasema Wanjara.
Anasema kutokana na kuwapo kwa gugu hilo katika Mkoa wa Pwani, anasema kuwa kiwango cha uzalishaji kimekuwa kikisuasua na kusabaisha wakulima kupata mavuno kidogo.
“Katika mkoa wetu huu wa Pwani zao tunalolitegemea kwa ajili ya biashara ni korosho likifuatiwa na muhogo, matunda, na mbogamboga sasa linavyoathiriwa na gugu hilo linasababisha Mkoa wa Pwani uathirike kimapato,”amesema.


Wakulima wazungumzia gugu tegemezi
Niliweza kupata fursa ya kuzungumza na baadhi ya wakulima wa zao la korosho kutoka katika Kijiji cha Malendego kilichoko Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi juu ya namna wanavyolitambua hili gugutegemezi na njia wanazozitumia katika kukabiliana nalo Mkulima wa Kijiji cha Malendego wilayani Kilwa, mkoani Lindi, Omary Mtunyungu anasema gugutegemezi limemuathiri kiuchumi na kwamba umasikini unabisha hodi katika familia yake.
Mtunyungu anasema kutokana na hali hiyo ametoa taarifa kwa wataalamu wa kilimo ili kupata msaada wa ufumbuzi, lakini mpaka sasa tatizo halijatatuliwa.
“Inaonekana idadi ya wataalamu wa kilimo ni ndogo kwa sababu sisi wa huku kijijini hatufikiwi na huduma hiyo naomba serikali ijitahidi kuongeza idadi ya wataalamu ili watusaidie jinsi ya kukabiliana na vikwazo vya kilimo hasa magonjwa .
Mkulima na mkazi wa Kijiji hicho cha Malendego, Mohamedi Mtauka anasema amekata tamaa kuongeza kilimo cha zao hilo kwa kuwa gugutegezi limeathiri sana mimea yake ya korosho na kusababisha kipato chake kushuka.
Asili ya kilimo cha zao la korosho ni kutoka nchi ya Brazil iliyopo Amerika ya Kusini na liliingizwa Tanzania katika karne ya 16 kutokea Msumbiji ambako lilikuwa likilimwa na Wareno.